Mshambuliaji wa Liverpool Mohamed Salah amemwambia mchezaji mwenzake, mlinda lango Loris Karius "kuwapuuza wapenda chuki" baada yake kukosolewa zaidi kutokana na makosa aliyoyatenda wakati wa mechi ya kuanza kwa msimu.
Karius, 25, alidaiwa kusababisha bao la tatu la Borussia Dortmund katika mechi ambayo Liverpool walilazwa 3-1.
Kipa huyo alielekeza mkwaju kutoka kwa Christian Pulisic wa Dortmund kwenye njia ya Bruun Larsen aliyefunga bao lao la ushindi.
Alifanya kosa hilo siku chache baada yake kudaiwa kufanya kosa jingine mapema mwezi huu mechi ya kirafiki dhidi ya Tranmere.
Alishindwa kudhibiti vyema mpira wa frikiki aliokuwa ameudaka na kuwawezesha wenyeji kufunga wakati wa mechi hiyo iliyomalizika kwa ushindi wa Liverpool wa 3-2 uwanjani Prenton Park.
Liverpool walikuwa wameongoza 3-0 kufikia wakati wa mapumziko kupitia mabao ya Rafael Camacho, Sheyi Ojo na Adam Lallana, kabla ya Jonny Smith na Amadou Soukouna kuwafungia Tranmere.
Meneja Jurgen Klopp baada ya mechi alisema: "Makosa hutokea; Huwa siyapendi, na yeye pia hayapendi."
Mwezi Mei, Mjerumani huyo alifanya makosa mawili makubwa wakati wa fainali ya Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya ambapo walishindwa na Real Madrid.
"Kuwa na nguvu Karius, hili limewahi kutokea kwa wachezaji wazuri zaidi," ameandika Salah.
Karius alikuwa awali amejibu shutuma zilizoelekezwa kwake kupitia ujumbe kwenye mtandao wa Instagram.
"Kwa wale wanaofurahia kuwaona watu wengine wakishindwa au kuteseka, nawaonea huruma," aliandika.
"Kile kinachotokea katika maisha yenu kuwafanya kuwa na chuki na hasira kiasi hiki, naomba kipite na mambo mema yatendeke kwenu."
Meneja wa Liverpool Jurgen Klopp amemtetea Karius lakini akaonya kwamba kipa huyo ataendelea kukosolewa hadi pale atakapocheza vyema sana kwa mechi kadha.
Liverpool wameimarisha safu yao ya ulinda lango kwa kumnunua kipa wa Brazil, Alisson, kutoka klabu ya Roma ya Italia.
Kushauriwa ahame
Karius, 24, alikuwa ameshauriwa ahamie taifa jingine kucheza soka baada ya makosa yake fainali ya Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya Jumamosi.
Kipa wa zamani wa England Robert Green ambaye mwenyewe aliwahi kufanya makosa kama hayo anasema: "Iwapo atarudi Ujerumani, ni kweli watu hawawezi kusahau alichokifanya lakini hataangaziwa zaidi."
"Kutoangaziwa sana kunaweza kuwa jambo zuri, kwenye ligi ya nyumbani, kwenda nje ya nchi ambapo watu hawakuwa wanajishughulisha sana na mechi hiyo."
Kosa la Green wakati wa Kombe la Dunia mwaka 2010 lilimfanya kufungwa bao rahisi na kusababisha mechi yao dhidi ya Marekani kumalizika 1-1.
Anasema tukio kama hilo linaweza kuwa ngumu sana kwa mlinda lango yeyote yule.
"nakumbuka baada ya Kombe la Dunia 2010 na mechi yangu ya kwanza ugenini Ligi ya Premia, kila nilipougusa mpira kulikuwa na watu kama 30,000 hivi uwanjani walikuwa wanapiga mbinja," anasema Green ambaye alichezea Norwich, West Ham, QPR na Leeds.
"Bahati mbaya kwa Karius ni kwamba nusu ya mechi ligini Uingereza ni za ugenini na anapokuwa upande wa mashabiki wageni hata uwanja wa Liverpool atakuwa anachekwa hata zaidi kama ugenini. Kipindi hiki cha kabla ya msimu kitakuwa kigumu sana kwake bila shaka.
"Makosa hutokea wakati wowote, yanaangazia zaidi unapokuwa mlinda lango ... lakini ukweli ni kwamba makosa yake yaliwagharimu ushindi mechi hiyo. Hilo litamkwamilia kwa muda lakini muhimu ni jinsi atakavyolipokea na natumai kwamba yeye kama binadamu na kipa ataweza kujikwamua na kurudi akiwa imara zaidi.
Chapisha Maoni