0
KAMATI ya Maudhui ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imetoa onyo kali kwa kituo cha Redio cha Times Fm, pamoja na faini ya kulipa kiasi cha Sh milioni 1, kutokana na kukiuka
vifungu vya maadili na kanuni za utangazaji, vilivyopo katika leseni ya utangazaji inayotolewa na mamlaka hiyo.

Akisoma hukumu hiyo jijini Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Margareth Munyagi, alisema ‘ Times Fm’ imepewa adhabu hiyo baada ya watangazaji wake kukiuka taratibu zilizowekwa na mamlaka hiyo, kwa kutangaza hewani maneno
yanayokiuka maadili ya utangazaji.
Munyagi alisema kwa nyakati tofauti kupitia kipindi chake cha ‘Hatua tatu’ kilichorushwa saa 3 hadi saa 5 asubuhi na ‘Mitikisiko ya Pwani’, kilichorushwa mchana wa Agosti 29 mwaka huu,
watangazaji wa vipindi hivyo walisikika
wakizungumzia dondoo zilizolenga kuhamasisha ngono bila kuzingatia muda huo ambao watoto wengi wanaweza kusikiliza.

Alisema kiutaratibu muda ambao dondoo hizo zilikuwa zikitangazwa, si muda muafaka kwa kuwa
vipindi hivyo pia vingewezwa kusikilizwa na watoto na kwamba muda wa dondoo kama hizo kutolewa unapaswa kuanzia saa 3 usiku hadi saa 11 alfajiri.

Aidha alisema utetezi uliotolewa na Mkurugenzi wa Redio hiyo, Leule Nyaulawa haukidhi haja mbali na kulipokea shitaka lililotolewa dhidi yao.
Nyaulawa alisema suala la kupata watangazaji wazuri Tanzania bado ni changamoto kutokana na
vyuo vingi kuzalisha watangazaji wasio na uwezo mzuri.

Pia alisema kupitia kwa utetezi wake watakwenda kulifanyia kazi suala hilo ili kuepusha kurudiwa kwa kosa kama hilo na mengine yaliyopo katika
leseni za utangazaji huku kamati hiyo ikitoa muda wa mwezi mmoja kwa Times Fm kulipa faini hiyo
au kukata rufaa kama haikuridhika na uamuzi uliotolewa dhidi yao.

Chapisha Maoni

 
Top