Chelsea imekubali kumuuza mlinda mlango wake raia wa Ubelgiji Thibaut Courtois Real Madrid huku ikihitaji nyongeza ya kiungo Mateo Kovacic kwa mkopo wa muda mrefu.
Chelsea inasema makubaliano hayo yanasubiri mazungumzo ya mwisho baina ya Courtois na Real Madrid sambamba na vipimo vya afya.
Madrid inatarajia kukamilisha usajili wa Courtois ambaye aliibuka mlinda mlango bora kwenye kombe la dunia kabla ya muda wa usajili kufikia kikomo Alhamisi.
Mlinda mlango wa Athletic Bilbao Kepa Arrizabalaga, anatarajiwa kuziba pengo ndani ya Chelsea kwa ada ya Paundi milioni 71, hii ikiwa ni rekodi mpya na ya juu zaidi kwa nafasi hiyo.
Kiungo wa Croatia Kovacic , 24, atafanyiwa vipimo vya afya siku ya Jumatano kabla ya kujiunga na miamba hiyo ya London kwa mkopo wa muda mrefu.
Amedumu Madrid kwa misimu mitatu akitokea Inter Milan ya Italia, akiwa pia katika kikosi cha Croatia kilichofika fainali kombe la dunia.
Courtois amekua mchezaji wa Chelsea tokea mwaka 2011 alipojiunga nayo akitokea Genk.
Alielekea Atletico Madrid kwa mkopo mpaka mwaka 2014 aliporejea darajani kama mchezaji namba moja katika nafasi ya mlinda mlango.
Alikosekana katika mazoezi siku ya Jumatatu baada ya kuwa mapumzikoni kufuatia kushriki kombe la dunia.
Kepa, 23, anatarajiwa kuwasili Stamford Bridge huku akiufunika usajili wa mlinda mlango mpya wa Liverpool Alisson aliyejiunga kwa ada ya Paundi Milioni 66 tokea Roma.
Ni mlinda mlango namba mbili kwenye timu ya taifa ya Hispania akiwa nyuma ya David de Gea wa Manchester United huku akicheza mpambano mmoja wa kimataifa.
Chapisha Maoni