Kocha Mkuu wa Mtibwa Sugar, Zubeir Katwila amesema kuwa mchezo baina yao na Simba ambao umepigwa leo kwenye dimba la Taifa jijini Dar es Salaam ulikuwa na lengo la kukiongezea kikosi chake uwezo wa kujiamini.
Mtibwa Sugar imelala kwa bao 1-0 kwenye mchezo huo lililolofungwa na Emmanuel Okwi dakika ya 45 ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kuanza kwa mtanange wa Ligi Kuu Soka Tanzania bara.
Akiongea baada ya kumalizika kwa mchezo huo, Katwila amesema kuwa mechi hiyo ilikuwa n kipimo sahihi kwa wachezaji kwa kikosi chake ambacho kina wachezaji wapya wengi.
“Mchezo kwa ujumla ulikuwa mzuri na kilikuwa ni kipimo kizuri kwetu sisi, kipimo ambacho nilikuwa nakitafuta na nimekipata, wachezaji wangu kama unavyowaona ni ingizo jipya kwa hiyo ni kipimo kizuri kabisa kabla ya ligi kuanza nimekipata”, alisema Katwila
Kujiamini
Katwila ambaye aliwahi kukichezea kikosi hicho cha Mtibwa Sugar kwa mafanikio amesema walikuwa na lengo la kutafuta uwezo wa kujiamini miongoni mwa wachezaji wake kwenye mchezo wa leo.
“Tulikuwa tunatafuta uwezo wa kujiamini miongoni mwa wachezaji dhidi ya timu kubwa kama ile (Simba), unaona kuwa wametufunga, lakini sio tatizo sana tumefungwa goli umeona makosa ya kawaida ambayo yanaweza kurekebishika lakini kwa ujumla nilikuwa naangalia kikosi changu tuna uwezo gani wa kucheza muda mrefu dakika 90 hadi na 120”, alisema.
Msimu Mpya
Na je, vipi kuhusu matarajio ya Mtibwa Sugar kuelekea msimu mpya wa VPL ambapo wataanza kwa kupepetana na Stand United kwenye uwanja wa Manungu-Turiani Agosti 26?
“Cha msingi ni kuwa sawasawa tu kwani muda wa maandalizi bado upo. Matarajio ni kufanya vizuri kwani hakuna mtu anayejiandaa kufeli kwahiyo sisi matarajio yetu ni kufanya vizuri kwa ajili ya kutafuta alama tatu ambazo ndizo zitatuweka pale juu”.
“Kadri unavyocheza zile mechi muhimu na kushinda na kupata alama tatu, ukikosa tatu pata hata moja kuliko kupoteza kabisa”, alimalizia Katwila.
Mtibwa Sugar wamepoteza mechi yao ya kirafiki dhidi ya Simba leo kwenye dimba la Taifa jijini Dar es Salaam kwa bao 1-0 lililofungwa na Emmanuel Okwi.
Jisajili kwenye:
Chapisha Maoni (Atom)
Chapisha Maoni