0
NAHODHA wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta amefunga mabao matatu timu yake KRC Genk ikiibuka na ushindi wa 5-2 dhidi ya Brondby IF ya Denmark katika mchezo wa kwanza wa hatua ya mwisho wa mchujo wa kuwania kuingia hatua ya makundi ya Europa League.
Katika mchezo huo uliofanyika Uwanja wa Luminus Arena mjini Genk, Samatta amefunga mabao yake katika dakika za 37, 55 na 70 wakati mabao mengine ya Genk yamefungwa na mshambuliaji Mbelgiji, Leandro Trossard kwa penalti dakika ya 45 na ushei na 90 na ushei.

Mabao ya wageni yamefungwa na beki wa Iceland, Hjortur Hermannsson dakika ya 47 na mshambuliaji Mpoland Kamil Wilczek dakika ya 51.
Genk sasa watatakiwa kwenda kuulinda ushindi wao katika mchezo wa marudiano ugenini, Agosti 30 Uwanja wa Brondby.
Kikosi cha KRC Genk kilikuwa: Vukovic, Uronen, Lucumi, Dewaest, Maehle, Berge, Malinovskyi, Pozuelo, Trossard, Samatta na Ndongala/Paintsil dk73.
Brondby IF : Schwäbe, Jung, Hermansson, Kaiser/Tibbling dk78, Mukhtar, Larsson, Wilczek, Christensen/Fisker dk88, Radosevic, Arajuuri na Erceg/Uhre dk70.

Chapisha Maoni

 
Top